Mhasibu feki atiwa mbaroni kwa wizi wa Tsh. 873,000
Na Nathaniel Limu, Singida
 Mhasibu
 wa hospitali ya mkoa mjini Singida aliyeachishwa kazi kwa kosa la 
kumiliki vyeti feki, Edith Talasi (49) mkazi wa Minga,anashikiliwa na 
jeshi la polisi kwa tuhuma ya kuvunja milango ya ofisi yake ya zamani na
 kuiba shilingi 873,000 taslimu, kwa kutumia funguo bandia.
Talasi 
 ambaye imelelezwa kwamba alifanya kazi hospitalini hapo kwa  muda na 
baadaye alirejeshwa kwenye kituo chake cha kazi manispaa ya 
Singida,kwenye wizi huo, alimshirikisha mlinzi wake wa nyumba ya kulala 
wageni Nandau, Antony Felix (51).Mlinzi huyo naye anashikiliwa na 
polisi.
Akizungumza
 na waandishi wa habari ofisini kwake Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani 
hapa, ACP Debora Magiligimba, alisema tukio hilo limetendeka Novemba, 21
 saa 6.30 usiku huko katika hospitali ya mkoa mjini hapa.
Alisema
 siku ya tukio muuguzi wa zamu Shamir Omari (27) akitokea maeneo ya 
mapokezi akielekea wodini, alimwona mtu akiwa amesimama karibu na ofisi 
ya mhasibu, alisimama akamsalimia na mtu huyo aliondoka.
“Muuguzi
 huyo aliamini kuwa mtu aliyemwona,huenda alikuwa  mgonjwa au mtu 
aliyeleta mgonjwa hospitalini.Lakini aliporudi,alimwona mtu yule yule 
amerudi eneo lile lile, kitendo kilichopelekea amshuku kuwa sio mtu 
mzuri,” alisema kamanda huyo.
Alisema
 muuguzi huyo baada ya kumtilia shaka mtu huyo, alitoa taarifa kwa 
mlinzi wa zamu wa hospitali hiyo, Abubakari Jumanne,ambaye alimweka 
chini ya ulinzi mtu huyo.
ACP
 Magiligimba alisema hata hivyo mtu huyo alijitetea kuwa amefika 
hospitalini hapo, kwa ajili kuchoma sindano na kuonyesha dawa ya unga na
 kichanganyio chake.
“Wakati
 wanaendelea na mahojiano hayo,waliona makufuli  mawili ya mlango wa 
nje/grili yapo chini na mlango huo wa chuma upo wazi. Mtuhumiwa mlinzi 
Antony alieleza kuwa bosi wake (mtuhumiwa Edith) kwa wakati huo,alikuwa 
ndani ya ofisi ya mhasibu amejifungia ndani,” alisema.
 Akifafanua 
 alisema  jeshi la polisi baada ya kupata taarifa ya wizi huo, liliweza 
kufika eneo la tukio na kukuta mlango wa ndani ukiwa umefungwa kwa 
ndani.
“Walipoamuru
 mhasibu afungue mlango huo kwa kutumia funguo zake,walimkuta mtuhumiwa 
(Edith) akiwa amejibanza kwenye kona ya mlango na watumishi wa hospitali
 hiyo, waliweza kumtambua. Alipohojiwa ameingiaje humo ndani,alionyesha 
funguo saba (07) na zilipojaribiwa ziliweza kufungua milango yote ya 
ofisi ya mhasibu,” alisema Magiligimba.
Alisema
 pamoja na wizi huo wa shilingi 873,000,imeelezwa kwamba aprili mwaka 
huu,wahasibu wa hospitali hiyo,walibaini upotevu wa shilingi 
1,800,000.Oktoba mwaka huu,pia walibaini upotevu wa shilingi 3,600,000.
Kaimu
 mganga mfawidhi wa hospitali hiyo, Dk. David Mwasita,amekiri kutokea 
upotevu huo lakini wahasibu katika wakati huo,waliweza kuziba upotevu 
huo, kwa fedha zao za mishahara.
Ameeleza
 kuwa wahasibu hao walilazimika kutoa fedha zao binafsi, na wasingeweza 
kutoa taarifa ya upotevu huo, kwa vile milango na kasiki, ilikuwa 
imefungwa kama kawaida.
ACP
 Magiligimba amesema kwa sasa wanaendelea kuwahoji watuhumiwa hao na 
baada ya kumalizika kwa mahojiano hayo,watuhumiwa watafikishwa 
mahakamani kujibu tuhuma inayowakabili.