Asimulia mkasa mzima wa vifo vya mumewe na watoto wake Kawe
Mama
 wa familia iliyouawa katika ajali ya kifusi iliyoua watu watano jijini 
Dar es Salaam wakiwemo baba na watoto wake wawili na binti wao wa kazi, 
Gaudensia Ephraim alinusurika baada ya yeye kudamkia katika biashara 
yake ya kukaanga maandazi.
Mume
 wa Gaudensia, Ephraim Manguli (47), watoto wake wawili Danford (5) na 
Fredy Ephraim (2) pamoja na binti wao wa kazi aliyetambulika kwa jina 
moja la Mariam, walikufa baada ya nyumba walimokuwa wakiishi kufunikwa 
na kifusi kwenye eneo la Kawe katika Manispaa ya Kinondoni, Dar es 
Salaam juzi asubuhi.
Baba
 mzazi wa Ephraim, Mzee Philemon Manguli alisema kama isingekuwa 
biashara hiyo na mkwewe angefariki katika ajali hiyo iliyotokea alfajiri
 ya Jumatano Aprili 6, mwaka huu na kusababisha vifo hivyo.
Alisema
 Gaudensia hufanya biashara ya kukaanga maandazi hivyo alidamka alfajiri
 kwenda katika biashara yake na wakati yupo huko alitaarifiwa kutokea 
kwa ajali hiyo na alipofika nyumbani akakuta nyumba imeanguka na familia
 yake imefukiwa.
“Mkwe
 wangu yeye hufanya biashara ya kukaanga maandazi, na wakati ajali 
inatokea tayari alikuwa katika biashara yake mtaa wa pili na 
alipoarifiwa na kurudi nyumbani ndio akakuta ajali hiyo ambayo iliua 
mumewe, watoto wawe wawili, binti yake wa kazi pamoja na mjukuu wa 
mwenye nyumba walimokuwa wakiishi,” alisema.
Akizungumza
 kwa niaba ya mkwewe ambaye hakuwa katika hali nzuri ya kuzungumza, 
Manguli alisema huenda mkwewe angefariki kama angekuwa ndani alfajiri 
ile, ila biashara yake ndiyo imemuokoa.
Manguli
 ameliambia gazeti hili kuwa msiba huo wa kijana wake aliyekuwa akifanya
 kazi katika kampuni ya ulinzi ya Mahela Night Wash imempa jeraha ambalo
 hatokaa kulisahau maishani mwake.
“Siamini
 hadi sasa kama mwanangu amefariki pamoja na wajukuu zangu Danfod na 
Fredy, lakini ndio hivyo ni mapenzi ya Mungu, ila sijui la kufanya,” 
alisema kwa huzuni Mzee Manguli.
Alisema
 jambo lingine la kusikitisha kwao ni namna misiba ilivyomuandama kwani 
wiki moja iliyopita hapo hapo nyumbani kwake alifariki mdogo wake na 
kusafirisha hadi kijijini kwao Mahenge mkoani Morogoro kwa maziko.
“Ijumaa
 iliyopita mimi na marehemu mwanangu, tumerudi kutoka Mahenge kumzika 
baba yake mdogo, na leo tena matanga yamerejea hapa hapa kwangu,” 
alisema Manguli.
Kuhusu
 taratibu za mazishi, msemaji wa familia hiyo, Mchungaji Geoffrey 
Masanju alisema maandalizi yanaendelea na kutokana na hali ngumu ya 
familia hiyo kwa sasa kutokana na kufululiza kwa misiba hiyo, 
wanatarajia kuzika Jumamosi katika makaburi ya Kinondoni.
“Mazishi
 yanataraji kufanyika Jumamosi katika Makaburi ya Kinondoni, lakini 
kubwa zaidi tunasubiri michango kutoka kwa ndugu na jamaa pamoja na 
Ofisi ya Mbunge wa Kawe ili kufanikisha mazishi haya,” alisema Mchungaji
 Masanju.
Masanju
 alisema mawasiliano baina yao na wazazi wa binti wa kazi aliyemtaja kwa
 jina la Mariam mwenyeji wa Musoma mkoani Mara yanaendelea ili kufahamu 
kama naye atazikwa pamoja na wenzake au atasafirishwa ijapokuwa uwezo wa
 kusafirisha kama wao kwa sasa ni mdogo.
Alisema
 msaada mkubwa wanaoutegemea wa kufanikisha maziko hayo ni kutoka kwa 
Mbunge wa Kawe, Halima Mdee ambaye tangu kutokea kwa tukio alituma 
mwakilishi wake ili kusaidiana na familia.






 





















 
    
 


Post a Comment Blogger Facebook