Baadhi ya benki nchini zinadaiwa kuajiri baadhi ya wafanyakazi walio 
kwenye mtandao wa majambazi kutokana na wateja wengi kupigwa risasi na 
kufa wakitoka kuchukua pesa, uchunguzi wa baadhi ya askari wa Jeshi la 
Polisi Tanzania umebaini.
Hayo yalisemwa na baadhi ya askari hao wiki iliyopita walipozungumza na 
mwandishi wetu na kusema kwamba, waajiri wasipokuwa makini katika 
kuajiri watashangaa kuona wateja wao wanapigwa risasi na kuuawa kila 
kukicha.
“Haiwezekani kuwa wanaonyang’anywa fedha ni wale wanaotoka kuchukua 
benki kuliko wanaopeleka! Ina maana wezi wapo katika baadhi ya mabenki 
hivyo kunatakiwa kuwepo na umakini wakati wa kuwaajiri,” alisema askari 
mmoja kutoka makao makuu ya jeshi hilo, Dar akiomba hifadhi ya jina lake
 kwa vile yeye si msemaji.
Afande huyo aliendelea kusema kuwa, baadhi ya wafanyakazi wasio 
waaminifu wa benki hizo wanapoona mteja anachukua fedha nyingi hufanya 
mawasiliano kwa njia ya simu kuwaeleza majambazi walio nje namna 
alivyovaa mteja huyo na kiasi cha fedha alichochukua.
Uchunguzi zaidi unaonesha kuwa, endapo hali hiyo haitadhibitiwa haraka 
huenda wananchi wakapatwa na hofu ya kuweka fedha zao benki kwa kuogopa 
kuporwa na kupigwa risasi wakienda kuzichukua.
 Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, DCP Simon Sirro 
(pichani) ambapo alikiri kuwepo kwa baadhi ya wafanyakazi wenye mtandao 
na majambazi huku akisema jeshi lake limeweka mikakati kuhakikisha 
mtandao huo unasambaratishwa mara moja.
“Ni kweli kwamba, baadhi ya mabenki, si yote, yameajiri baadhi ya 
wafanyakazi, si wote wenye mtandao na majambazi. Kwa hiyo hata wao ni 
majambazi tu.
“Sasa tumejipanga vizuri ikiwa ni pamoja na kukamata pikipiki 
zinazohusika katika uhalifu. Pia tumeamua kuweka makachero nje na ndani 
ya mabenki, wapo polisi wa miguu, pikip iki na magari. Nina uhakika 
tutawadhibiti,” alisema Kamanda Sirro.
Aliendelea kusema kuwa, majambazi waliopo katika Kanda ya Dar es Salaam 
waanze kufunga virago kwani bila kufanya hivyo wajue watakamatwa wote na
 mtandao wao kumalizika. Pia aliwataka wamiliki wa mabenki kuwa makini 
wakati wa kuajiri wafanyakazi ili kuwapata wenye sifa njema na kuweka 
imani kwa wateja wao.
Aliyekuwa Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Kamishina 
Suleiman Kova aliwahi kutamka kuwa, baadhi ya wafanyakazi wa ndani wa 
baadhi ya benki wana ushirikiano na majambazi. Akawatahadharisha 
wamiliki kuwa makini wakati wa kuajiri.