 
UMOJA WA KATIBA YA WANANCHI (UKAWA),
DAR ES SALAAM,
TANZANIA.
TAARIFA KWA UMMA,
DAR ES SALAAM, ALHAMIS, 30 APRIL 2015
UCHAGUZI MKUU OKTOBA 2015 LAZIMA, KIKWETE ASIONGEZEWE MUDA, KURA YA MAONI BAADAE
Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) leo vimetoa 
msimamo wao juu ya njama za kuahirisha Uchaguzi Mkuu unaotakiwa 
kufanyika Oktoba mwaka huu. UKAWA imesisitiza kwamba kuahirisha Uchaguzi
 Mkuu huo ni sawa na kumuongezea Rais Jakaya Kikwete na Chama chake cha 
Mapinduzi muda wa kuendelea kutawala Tanzania. UKAWA imesema jaribio 
lolote la kuahirisha Uchaguzi Mkuu kwa kisingizio chochote kile litakuwa
 kinyume na Katiba ya sasa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na 
litahesabika kuwa ni sawa na mapinduzi dhidi ya Katiba (constitutional 
coup d’etat). Msimamo wa UKAWA unafuatia kumalizika kwa Kikao cha 
Viongozi Wakuu wa Vyama vinavyounda UKAWA (UKAWA Summit) kilichofanyika 
katika Makao Makuu ya Chama cha Wananchi (CUF), jijini Dar es Salaam 
kati ya tarehe 28 na 29 Aprili mwaka huu.
Akielezea msimamo wa UKAWA juu ya suala hili, mwenyeji wa Kikao hicho na
 Mwenyekiti wa CUF Profesa Ibrahim Lipumba alisema kwamba kuna dalili za
 kuonyesha kwamba zipo njama za kuahirisha Uchaguzi Mkuu na kumuongezea 
Rais Kikwete na CCM muda wa kutawala. “Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) 
haijaanza maandalizi yoyote kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu licha ya kwamba 
imebaki miezi sita tu Uchaguzi huo ufanyike kwa mujibu wa Katiba. 
Shughuli zinazohusiana na maandalizi ya Uchaguzi Mkuu na vifaa 
vinavyotumika kwa ajili yake ambavyo kwa taratibu za miaka yote huanza 
kufanyika angalau mwaka mmoja na nusu kabla ya Siku ya Uchaguzi 
hazijaanza kufanyika, vifaa vinavyohitajika havijanunuliwa na fedha kwa 
ajili hiyo hazijatengwa hadi sasa.”
Profesa Lipumba aliongeza kwamba jambo hili limefanyika kwa makusudi kwa
 sababu vyama vya UKAWA vimekuwa vinapigia kelele suala la maandalizi ya
 Uchaguzi Mkuu tangu mwaka 2012. “Licha ya madai ya muda mrefu ya Kambi 
Rasmi ya Upinzani Bungeni kwamba ratiba ya Uchaguzi Mkuu wa 2015 
imevurugwa kwa makusudi kwa kutokutenga fedha kwa ajili hiyo katika 
bajeti ya Serikali tangu mwaka 2012, Serikali hii ya CCM haijatoa fedha 
kwa NEC kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu. Badala yake, NEC imeendelea 
kutangaza kwamba inafanya maandalizi kwa ajili ya Kura ya Maoni kuhusu 
Katiba Inayopendekezwa ambayo imepitwa na muda kisheria na haiwezi 
kufanyika tena bila kwanza kufanyika kwa marekebisho katika Sheria ya 
Kura ya Maoni (the Referendum Act) ya mwaka 2013.”
Kwa mujibu wa Profesa Lipumba, Kura ya Maoni ilitakiwa ifanyike ndani ya
 siku 124 kutoka tarehe Rais Kikwete alipotoa Tangazo la Kura ya Maoni 
na kutamka kuwa Kura hiyo itafanyika tarehe 30 Aprili, 2015, yaani leo. 
Profesa Lipumba alisema: “Kwa Sheria ya Kura ya Maoni ilivyo kwa sasa, 
hakuna uwezekano wa Kura ya Maoni kufanyika tena bila kwanza kufanya 
marekebisho ya Sheria hiyo. Kila hatua inayotakiwa kuchukuliwa chini ya 
Sheria hiyo imewekewa muda wake na muda huo haubadiliki. Tangazo la Kura
 ya Maoni likishatolewa na tarehe kutangazwa haibadilishwi kwa sababu 
yoyote ile. Hakuna namna yoyote ya kuahirisha Kura ya Maoni na kuifanya 
tarehe nyingine yoyote.”
Profesa Lipumba aliongeza: “Haya ndio masharti ya Sheria ya Kura ya 
Maoni. Yasipofuatwa hakuna namna ya kuyarekebisha bila kwanza 
kurekebisha Sheria yenyewe. Na hadi sasa Serikali hii ya CCM haijapeleka
 Muswada wa Sheria kuirekebisha Sheria hiyo ili kuwezesha Kura ya Maoni 
kufanyika kwa tarehe nyingine. Tunashangazwa na Tume inayoongozwa na 
aliyekuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani ambayo ndio mahakama ya juu kabisa 
katika nchi yetu, na Mkurugenzi wa Uchaguzi ambaye ni Mwanasheria 
Mwandamizi wa Serikali, kuendelea kutangaza kwamba Kura ya Maoni 
itafanyika kwa terehe itakayotangazwa baadae wakati Tume inafahamu 
kwamba jambo hilo haliwezekani kisheria. Kama bado CCM na washirika wake
 wanataka Katiba Inayopendekezwa ipigiwe Kura ya Maoni na Watanzania ni 
lazima wapeleke Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Kura ya Maoni 
Bungeni. Vinginevyo itakuwa na ubatilifu mtupu kama tuliouona wakati wa 
Bunge Maalum.”
Aidha, UKAWA imesema haiko na haitakuwa tayari kuunga mkono jitihada 
zozote za kumuongezea Rais Kikwete na CCM muda wa kutawala kwa 
kuahirisha Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu. Kwa mujibu wa Mwenyekiti Mwenza 
wa UKAWA na Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, Mheshimiwa James 
Mbatia, haijawahi kutokea Uchaguzi Mkuu ukaahirishwa kwa sababu yoyote 
tangu mwaka 1960 tulipofanya Uchaguzi Mkuu uliotupatia Serikali ya 
Madaraka ya Ndani hadi sasa.
Mheshimiwa Mbatia alisema: “Watu hawa wanafahamu kuwa tumekuwa tukifanya
 Uchaguzi Mkuu kila baada ya miaka mitano tangu mwaka 1960. Hata mwaka 
1980, miezi michache baada ya kutoka vitani dhidi ya nduli Iddi Amin wa 
Uganda na licha ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere kutangaza miezi 18 ya 
kujifunga mikanda kwa sababu ya hali mbaya ya uchumi iliyosababishwa na 
Vita ya Uganda, hatukuahirisha Uchaguzi Mkuu wa mwaka huo. Watu hawa 
wanafahamu kwamba Katiba yetu hairuhusu Uchaguzi Mkuu kuahirishwa kwa 
sababu yoyote ile. 
Wanafahamu kwamba tangu mwaka 1985, Rais anatakiwa atumikie vipindi 
viwili tu vya miaka mitano mitano. Wanafahamu kwamba maisha ya Bunge ni 
miezi sitini au miaka mitano kuanzia tarehe ya Uchaguzi Mkuu na 
haiwezekani kwa maisha hayo kuongezewa muda kikatiba bila ya kufanyika 
Uchaguzi Mkuu. Na wanafahamu kwamba Rais Kikwete anakamilisha kipindi 
chake cha pili mwezi Oktoba mwaka huu na maisha ya Bunge la Kumi 
yanamalizika mwezi huo. Kuruhusu Uchaguzi Mkuu uahirishwe kwa kisingizio
 chochote kile ni kuwazawadia wazembe na kuwaongezea mafisadi 
wanaolimaliza taifa letu kwa ufisadi muda wa kuendelea na ufisadi huo. 
UKAWA haitakubali kuruhusu jambo hilo litokee.”
Aidha, UKAWA imesisitiza kwamba haitakubali na haitaunga mkono jaribio 
lolote la kufanya marekebisho katika Katiba ya sasa kwa lengo la 
kumuongezea Kikwete, chama chake na Serikali muda wa kutawala. Akielezea
 msimamo huo, Mwenyekiti Mwenza wa UKAWA na Mwenyekiti wa chama cha 
National League for Democracy (NLD) Dkt. Emmanuel Makaidi amesisitiza 
kwamba suala la vipindi viwili vya miaka mitano mitano kwa Rais wa 
Jamhuri ya Muungano ni nguzo kuu muhimu ya Katiba ya sasa na UKAWA 
haitakubali nguzo hiyo iguswe au kufumuliwa kwa sababu au kisingizio 
chochote kile. Dkt. Makaidi alisema: “Kubadilisha Katiba ya sasa kwa 
lengo la kuahirisha Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka sio tu kutaathiri 
misingi muhimu ya Katiba ya sasa, bali pia kutahatarisha amani ya nchi 
yetu. Tumeona kinachoendelea Burundi baada ya Rais Pierre Nkurunzinza na
 chama chake kuamua kujiongezea muda wa kutawala nchi hiyo. Tumeona 
yanaoendelea Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) baada ya Joseph 
Kabila kutaka kufanya hivyo hivyo. Kikwete na wanaCCM wenzake wasitake 
kuiingiza nchi yetu katika majanga yasiyokuwa na sababu.”
Kwa upande mwingine, UKAWA imeitaka NEC kuhakikisha kwamba wananchi wote
 wenye sifa ya kuandikishwa kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura 
wanaandikishwa kwenye Daftari hilo. Katika Mkutano wake na vyama vya 
siasa uliofanyika Dar es Salaam tarehe 9 Julai mwaka jana, Mwenyekiti wa
 Tume Jaji Damian Lubuva alisisitiza kwamba NEC ilikuwa na uwezo na 
vifaa vya kuandikisha takriban wapiga kura milioni 24 katika vituo vya 
kuandikishia 40,000 nchi nzima kwa muda wa siku 14 katika kila kituo cha
 kuandikishia. Mwenyekiti Mwenza wa UKAWA na Mwenyekiti wa CHADEMA 
Mheshimiwa Freeman Mbowe alieleza kushangazwa kwa UKAWA na matamko ya 
Tume kwamba sasa Tume itaandikisha wapiga kura kwa muda wa siku saba 
katika kila kituo.
Mwenyekiti Mbowe alisema: “Tume iliwaahidi Watanzania kwamba watu wote 
wenye sifa wataandikishwa katika Daftari la Wapiga Kura. Sisi wa UKAWA 
tulishauri muda wa kuandikisha uongezwe hadi angalau siku 28 kama 
ilivyokuwa kwa Uchaguzi Mkuu uliopita lakini Tume iling’ang’ania kwamba 
muda wa siku 14 unatosha. Leo Tume inapunguza muda huo wakati tunafahamu
 kwamba Tume ina vifaa pungufu vya kuandikishia wapiga kura kuliko 
ilivyoomba kupatiwa na Serikali hii ya CCM. Hii ni njama ya Tume na ya 
Serikali hii ya CCM kuhakikisha wapiga kura wengi hawaandikishwi. Sisi 
UKAWA hatutakubali jambo hilo litokee.”
Wakati huo huo, Viongozi Wakuu wa UKAWA wameeleza kushangazwa na taarifa
 zilizosambazwa na baadhi ya vyombo vya habari hapa nchini kwamba Chama 
cha NCCR-Mageuzi kimejitoa au kimeandika barua ya kuomba kujitoa kwenye 
UKAWA. Viongozi hao wamesema kwamba taarifa hizo ni uzushi mtupu 
unaosambazwa na wapiga ramli na wanajimu wa kiama cha UKAWA kwa lengo la
 kuipatia CCM na vyama vibaraka wake ahueni ya kisiasa. Akikanusha 
taarifa hizo, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi Mheshimiwa Mbatia amesema 
kwamba yeye mwenyewe na Katibu Mkuu wake Mosena Nyambabe pamoja na 
maafisa wa chama chake wamekuwa katika hatua zote za vikao vya UKAWA 
kuanzia Kamati ya Ufundi na ile ya Wataalam hadi Kikao cha Viongozi 
Wakuu kilichomalizika jana.
Mheshimiwa Mbatia alisisitiza: “Tangu juzi tupo hapa tukijadiliana namna
 ya kupata wagombea wa UKAWA wa ngazi zote kuanzia Urais, Ubunge hadi 
Udiwani. Kwa kiasi kikubwa tumeshakamilisha kazi ya kupata wagombea 
Ubunge wa UKAWA. Tumeshapata muafaka kwa zaidi ya asilimia 95 ya majimbo
 yote ya Uchaguzi Tanzania, na majimbo 12 yaliyobakia tunaendelea 
kuyashughulikia na tutayapatia ufumbuzi muda si mrefu. Tunaendelea na 
majadiliano juu kupata Mgombea Urais na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya 
Muungano atakayepeperusha bendera ya UKAWA. Tumeshakamilisha kazi hiyo 
kwa upande wa Zanzibar na tutaikamilisha kwa upande wa Jamhuri ya 
Muungano katika muda muafaka. UKAWA iko imara sasa kuliko kipindi 
kingine chochote tangu Bunge Maalum mwaka jana. Hao wanaosambaza uzushi 
kwamba tumefarakana na kwamba sisi NCCR tumejitoa au tunataka kujitoa 
watafute hoja nyingine. Hii imebuma.”
Mungu Ibariki Tanzania!
Imetolewa na;
---------------------------------------
Prof. Ibrahim Haruna Lipumba,
Mwenyekiti – CUF – Chama Cha Wananchi,
-----------------------------------
Mh.Freeman Mbowe (MB),
Mwenyekiti - CHADEMA
--------------------------------------
Mh.James Francis Mbatia(MB),
Mwenyekiti – NCCR MAGEUZI.
--------------------------------------
Mh. Dkt. Emmanuel Makaidi
Mwenyekiti – NLD.