Membe Arudisha Fomu Ya Urais......Akana Kuhusika Na Ufisadi Wa Mabilioni Ya Libya.
MAKADA maarufu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wamerejesha fomu na kufafanua mambo kadhaa ambayo yamekuwa yanazungumzwa juu yao kama njia ya kujiweka sawa kabla ya uteuzi kufanywa na vikao vikuu vya chama hicho.
Mmoja wa waliorudisha fomu ni Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye 
wakati akirudisha fomu za kuomba kuteuliwa na kusema kuwa wanaochukulia 
suala la urais ni la kufa au kupona wana matatizo kwani anayejua Rais wa
 Tanzania ajaye ni Mungu.
Alisema safari yake ya kutafuta wadhamini ilikuwa na misukosuko mingi
 ikiwemo kutokea ajali tatu lakini hakuna ambaye alikuwa ameumia sana.
Akiwa ameongozana na mke wake, Tunu Pinda alisema mwana CCM mkomavu ni yule ambaye yuko tayari kukubali matokeo.
Alisema mpaka sasa ni wanachama wa CCM 42 waliojitokeza kugombea 
lakini katika hatua ya kwanza ni majina matano tu yatakayoteuliwa na 
kundi kubwa litaondolewa.
“Mimi sitegemei kwenye mchujo wa watu watano watokee watu wa 
kunung’unika kwani kila mtu aliyefika kuchukua fomu alikuwa anafahamu 
kuwa kutakuwa na mchujo kama tuko wengi wako watano kisha unakwenda 
ngazi ya pili, hakuna sababu ya kunung’unika,” alisema.
Alisema baadaye kuna kwenda kwenye Mkutano Mkuu atabaki mmoja. 
“Utanung’unikia nini? Kuna kushinda na kushindwa na kuna kupata na 
kukosa na ukisema suala la Urais ni kufa au kupona basi una matatizo, 
ifike mahali wana CCM wapate mtu ambaye wanadhani anaweza kusaidia 
kuongoza,” alisema.
Pia alisema waliojitokeza mwaka huu kuchukua fomu ni wengi. 
“Tuliojitokeza tusinuniane, kwa nini haniungi mimi mkono, na wewe usione
 jambo hili ni nongwa na usijione mapenzi ya Mungu yako kwako tu,” 
alisema.
Pia aliwataka viongozi wenzake washirikiane kumuunga mkono mgombea 
mmoja atakayepeperusha bendera ya CCM. “Anayejua rais wa Tanzania 
atakuwa nani ni Mungu peke yake,” alisema.
Mwakyembe arudisha fomu
Waziri wa Afrika Mashariki, Dk Harrison Mwakyembe jana alirudisha 
fomu na kusema CCM itapata ushindi wa kishindo katika uchaguzi mkuu 
utakaofanyika Oktoba mwaka huu kutokana na kutekeleza ilani yake vizuri 
na wananchi kuwa na imani kubwa na chama hicho.
Mwakyembe ambaye alirudisha fomu jana mchana alisema katika safari 
yake ya kutafuta wadhamini mkoani ameweza kuwaona wanachama wengi wa CCM
 ambao wanaonesha imani kubwa na chama chao.
Alisema kila alipokutana na wana CCM waliojitokeza kumdhamini kwa 
tathmini aliyofanya tangu kuanza kwa siasa ya vyama vingi nchini CCM, 
itashinda ushindi wa kimbunga kwani mtaji upo kutokana na kazi kubwa 
iliyofanya serikali ya awamu ya nne katika utekelezaji wa ilani.
“Tumejipanga kuhakikisha wanaingia kwenye uchaguzi kifua mbele 
kutokana na kutekeleza ilani,” alisema. 
Pia alisema kwa upande wa pili 
wana kazi ya kuhakikisha yote mazuri yaliyofanywa na CCM yanasemwa.
 “Tuna kazi ya kuhakikisha kuwakumbusha wananchi barabara za lami na 
mafanikio mengi yamepatikana na serikali ya awamu ya nne ya CCM,” 
alisema.
Alisema kazi kubwa ni kuhakikisha umma unatambua CCM imefanya mambo 
mengi kutokana na upotoshaji unaofanywa na wapinzani kuwa CCM haijafanya
 lolote.
Pia alisema CCM kuwa na wagombea wengi waliojitokeza mwaka huu ni 
dalili njema za CCM kutoa fursa za kupatikana mmoja ambaye kila moja 
atamuunga mkono ili kuweza kukivusha chama.
Dk Mwakyembe alisema yuko tayari kumuunga mkono mgombea 
atakayeteuliwa na chama. Awali alisema amezunguka katika mikoa 15 katika
 kutafuta wadhamini.
Dk Mwele Malecela
Mwanachama mwingine wa CCM aliyerudisha fomu jana ni Dk Mwele 
Malecela ambaye alisema pamoja na kazi kubwa iliyofanywa katika uongozi 
wa awamu nne bado kuna watu wanaoishi kwenye umasikini uliokithiri.
Alitoa kauli hiyo wakati wa mkutano wake na waandishi wa habari. 
Alisema alifanikiwa kupata wadhamini katika mikoa 20 ikiwemo 17 ya 
Tanzania bara na mitatu ya Zanzibar.
Alisema wananchi wameonekana kufarijika kuona wanafuatwa kwenye 
maeneo ya kata walipo. Alisema ameweza kuzunguka mikoa tisa kwa siku nne
 hali inayoonesha kuwa kazi kubwa imefanyika katika ujenzi wa barabara 
za lami kuunganisha mikoa.
‘Pamoja na maendeleo na kazi kubwa ya awamu zote bado kuna umasikini 
uliokithiri lazima kuliangalia suala hilo kama kiongozi na kulitafutia 
ufumbuzi,” alisema.
Alisema aliguswa sana na wanawake waliojitokeza wakiwemo wazee ambao 
walikuwa wakitaka kumuona ni mwanamke wa aina gani ambaye anataka 
kugombea Urais.
“Wanawake wamefurahi sana kuona wanawake tunajitokeza hii ni fursa 
nzuri ya kuwapa moyo akinamama kugombea nafasi mbalimbali za uongozi 
katika nchi,” alisema.
Membe Ayakana  Mabilioni  ya  Libya
Membe kwa upande wake wakati anarudisha fomu akijibu swali 
aliloulizwa kuhusu madai ya kuwa anahusika na ufisadi wa fedha za Libya 
na kama inavyosambazwa na wapinzani wake, alisema akigundulika kuwa 
alikula hata dola moja yuko tayari kujiuzulu.
“Uvumi kuwa nahusika na mabilioni ya Libya hauna mashiko kabisa 
baadhi ya wanasiasa wenzangu wanajua ukweli wote huu lakini kwa makusudi
 wameamua kuniunganisha na kampuni hiyo na kuwaaminisha watu ni yangu au
 nina hisa maneno hayo ni ya uongo,” alisema.
Alifafanua kuwa Libya ni moja kati ya nchi wafadhili wa Tanzania 
ambapo, kama ilivyo wafadhili wengine imekuwa ikiipa Tanzania misaada na
 mikopo yenye masharti nafuu.
Alisema katika utaratibu huo, Tanzania na Libya zilitia sahihi 
mkataba wa kubadili madeni na kuyaingiza katika miradi ambao uliweka 
utaratibu wa matumizi na urejeshaji wa fedha za deni la Libya.
Alisema kumbukumbu alizonazo zinabainisha kuwa kabla ya Serikali ya 
Libya kuweka saini katika mkataba wa nyongeza iliyotaka fedha hizo 
zikopeshwe kwa kampuni ya Meis, upembuzi yakinifu wa mradi husika 
ulifanywa kupitia vyombo vyake, na wao wenyewe kujiridhisha juu ya ubora
 wa mradi huo.
Sumaye na mahakama ya rushwa
 Naye Waziri Mkuu mstaafu, Frederick 
Sumaye ambaye naye alirejesha fomu alisema akichagulia kuwa Rais wa nchi
 ataanzisha mahakama maalumu ya wala rushwa.
Mbali na rushwa pia vipaumbele vyake ni pamoja na ufisadi, uhujumu 
uchumi na kwamba ataunda chombo cha uchunguzi katika masuala hayo.
Pia alisema wakati akiwa Waziri Mkuu wa Tanzania alifanya mambo 
makubwa na atahakikisha anaunda serikali inayofahamu kutimiza wajibu 
wake.
‘Uchumi ninaouzungumzia si wa takwimu ni wa hali halisi, nitaangalia 
pia maeneo kama viwanda vikubwa na vidogo ili watu wengi waweze 
kujiajiri na kulinda viwanda vya ndani,” alisema.
Alisema atahakikisha uzalishaji wa viwanda vya ndani unaongezeka na 
kunakuwa na ongezeko la mauzo ya nje ya nchi. Pia alisema ataimarisha 
huduma za jamii, ikiwemo elimu, afya upatikanaji wa maji na huduma 
nyingine muhimu.
Alipohojiwa kama maeneo aliyokwenda kutafuta wadhamini aliombwa 
rushwa, Sumaye alisema, tangu aanze kazi ya siasa hajawahi kutoa rushwa.
“Hata maeneo ambayo nimekwenda kutafuta wadhamini sijatoa fedha hata 
zilizodaiwa kwa lugha laini nilikataa kwani nilitaka nidhaminiwe na wale
 walio na imani na mimi,” alisema.
Alisema wakati akiwa Waziri Mkuu alipambana na wala rushwa ambapo 
aliweza kuwafukuza kazi watu 3,360 huku wengine 400 walipelekwa 
mahakamani.
Balozi Mahiga
Balozi Mahiga naye wakati anarejesha fomu alisema ameenda mikoa 15 
kwa gari na akawashukuru wana CCM kumlaki na kwamba wamehamasika na 
wanasubiri kwa hamu uchaguzi.
Alisema kama CCM ikimpitisha kuwa mgombea atahakikisha kuwa anajenga 
maadili ya uongozi ili kuondokana na vitendo vya rushwa na ufisadi.
Alisema uongozi mzuri ni ule unaojengwa katika misingi ya maadili na 
atapambana na rushwa ili kukomesha vitendo hivyo ambavyo vimekuwa 
vikirudisha nyuma wananchi wengi.
“Nitahakikisha ninaimarisha misingi ya umoja na mshikamano katika 
nchi ikiwa ni pamoja na kudumisha muungano wa Tanzania na Zanzibar,” 
alisema.
Joseph Chaggama
Mwanachama mwingine wa CCM aliyerudisha fomu jana ni Joseph Chaggama 
ambaye alisema amezunguka katika mikoa 17 wakati wa kutafuta wadhamini. 
Alisema anaijua CCM vizuri na jinsi Serikali inavyoendeshwa.
Alisema yeye ni mmoja wa watu wasiofahamika na sababu ya kuchukua fomu ni nia ya dhati kutoka moyoni kuwa anaweza kuongoza nchi.
Pia alisema uwezekano wa yeye kuchaguliwa lazima kutokee muujiza. 
Alisema yuko tayari kuwatumikia Watanzania ikiwa atapewa ridhaa ya kuwa 
mgombea wa CCM na akashinda uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba mwaka 
huu.
Pia alisema yuko tayari kumuunga mkono mgombea ambaye atateuliwa na chama.
Monica Mbega
Mbunge wa zamani wa Iringa Mjini, Monica Mbega naye 
alirudisha fomu na kusema kuwa chama kiliweka utaratibu mzuri wakati 
wakienda mkoani kupata wadhamini katika mikoa 15 ikiwemo mitatu ya 
Zanzibar.
Alisema amekamilisha kazi yake kwa ukamilifu bila matatizo na kuwashukuru wanawake wengi waliojitokeza kumuunga mkono.
Alisema suala la rushwa linategemea jinsi mtu alivyokwenda wakati akitafuta wadhamini.
Amos akemea matumizi makubwa ya fedha
Mwingine aliyerudisha fomu 
hizo jana ni Amosi Siyantemi ambaye ni mtumishi wa CCM wakati ambaye 
alisema kuwa kwenye mchakato wa kutafuta wadhamini baadhi ya wagombea 
wameonesha matumizi makubwa ya fedha.
“Ni jambo la kujiuliza fedha hizo wamepata wapi na ni kiasi gani ni lazima wachunguzwe na kuchukuliwa hatua,” alisema Siyantemi.
Pia
 alisema rushwa ni ugonjwa mbaya unaoiangamiza jamii ni lazima 
zichukuliwe hatua za haraka na makusudi ili kuweza kukomesha suala hilo 
kabla nchi haijatumbukia kwenye shimo la machafuko.
Alisema CCM ya sasa si kama ile ya Mwalimu Nyerere. “Tunahitaji 
kurejesha haraka heshima ya CCM machoni mwa Watanzania na kwenye macho 
ya Jumuiya ya Kimataifa,” alisema.
Alisema akichaguliwa kuwa Rais atahakikisha kunakuwa na huduma bora 
za matibabu sanjari na bima ya afya kwa kila Mtanzania, kufanya 
mabadiliko makubwa kwenye mfumo wa elimu kwa kuchukua hatua mbalimbali 
ikiwemo kupunguza idadi ya masomo.
Pia alisema atapiga marufuku mauzo na manunuzi yanayofanyika nchini 
kwa malipo ya dola ambapo malipo ya dola yatafanyika kwa kibali maalumu.
Pia alisema atakuwa na jukumu la kuleta mageuzi makubwa katika sekta 
ya sanaa, michezo na burudani yatakayolenga kuwanufaisha kiuchumi 
wananchi. 

 


